Kero Mbalimbali Zatatuliwa
*Watumushi Wapongeza zoezi hilo*
Watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Sengerema wametakiwa kudai haki zao za kiutumishi wawapo katika utumishi na kuepuka kusubiri wakati wa kustaafu.
Wito huo umetolewa leo Aprili 28, 2025 na Katibu Tawala Wilaya ya Sengerema Ndugu Curthbert Midala kwenye kikao cha kusikiliza na kutatua kero za watumishi mbalimbali wa tarafa ya Sengerema kilichoandaliwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Sengerema na kufanyika kwenye ukumbi wa Sekondari ya Sengerema.
Kupitia kikao hicho Katibu Tawala Wilaya amewataka watumishi hao kutokuchoka kudai haki zao wawapo katika utumishi kwani kupitia utatuzi wa changamoto hizo kutasababisha utendaji kazi mahili kwa watumishi sambamba na utatuzi wa kero mbalimbali za wananchi kwenye ngazi za vijiji kwa wakati.
"Mambo yetu sisi watumishi tuyafuatilie wakati tupo katika utumishi tusisubiri tumestaafu ndiyo tuanze kufuatilia madai na vitu vingine, lakini pia sisi watumishi katika utumishi wetu tunatakiwa tuwe sehemu ya utatuzi wa changamoto za wananchi huko vijijini badala ya kupeleka matatizo yote kwa viongozi wa Wilaya" amesema Katibu Tawala Wilaya.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Sengerema Binuru Shekidele amesema kumekuwa na tabia ya baadhi ya watumishi waliopo makao makuu ya Halmashauri kutumia lugha chafu kwa watumishi wengine hususan waliopo vijijini ambapo amekemea vikali tabia hiyo na kuahidi kuchukua hatua kali kwa watumishi wenye tabia hizo.
Mkurugenzi Mtendaji amesikiliza kero mbalimbali na kuzipatia ufumbuzi kupitia kikao hicho ambapo amesema kero zilizobaki ambazo zipo ndani ya uwezo wa Halmashauri zitatatuliwa na zile zinazohusiana na Serikali kuu zitafikishwa kunakohusika kwa wakati.
Watumishi mbalimbali waliofika katika kikao hicho wamepongeza juhudi hizo za Mkurugenzi Mtendaji kuamua kusikiliza kero za watumishi na kuzipatia ufumbuzi papo hapo ambapo wameomba vikao kama hivyo vifanyike mara kwa mara.
Kupitia kikao hicho watumishi mbalimbali wametoa kero zao nyingi zikihusu madai mbalimbali ya uhamisho, upandishwaji wa madaraja, unadilishwaji wa miundo na maounjo ya mishahara.
Kikao kama hicho kitaendelea tena katika tarafa za Nyachenche na Katunguru ambapo watumishi wote wametakiwa kufika na kuelezea kero zao.
Sengerema District Council
Anuani ya Posta: Box 175
Simu ya Mezani: 028 2590162
Simu: 0688223308
Barua pepe: ded@sengeremadc.go.tz
Copyright ©2021 SENGEREMA DISTRICT COUNCIL . All rights reserved.